Mtandao huu bado upo kwenye matengenezo, punde utapata matukio katika picha, habari, makala na taarifa mbali za kijamii...Endelea kutufuatilia

Tuesday, April 17, 2018

WANAKIJIJI WALILIA KITUO CHA AFYA KATA YA ITEWE MBEYA



SERA ya afya ya mwaka 2007 imeelekeza kuwa kila kata inatakikwa kuwa na kituo cha afya na kila kijiji kuwa na Zahanati ili kurahisisha upatikanaji wa huduma za afya kwa wananchi hasa wanaoishi maeneo ya pembezoni.
Mkakati wa kufikia lengo la sera hiyo ni Serikali kushirikiana na wananchi pamoja na wadau wengine ambapo pia serikali inatakiwa kuhakikisha kunakuwepo na watoa huduma wa kutosha, vifaa tiba na dawa katika vituo vya kutolea huduma za afya.
Pia sera hiyo imesisitiza namna  Serikali itakaposhirikiana na wadau na wananchi katika juhudi za kupanua na kukarabati majengo ya kutolea huduma za afya pamoja na kuhakikisha kunakuwepo na  uwiano wa kijiografia katika kutoa huduma za afya nchini.
Utekelezwaji wa sera hiyo katika maeneo mengi hasa ya pembezoni mwa miji bado haujafanikiwa kwa kiwango kikubwa kutokana na kuwepo kwa changamoto lukuki za upatikanaji wa huduma za afya.
Miongoni mwa sehemu ambazo hazijaguswa na Tamko la Sera hiyo ni kata ya Itewe iliyopo katika halmashauri ya Wilaya ya Mbeya, ambayo ilianzishwa mwaka 2009, kutoka kwenye kata mama ya Iyela.
Kata ya Itewe ni Miongoni mwa kata 28 za halmashauri ya Mbeya vijijini ikiwa  ina jumla ya watu 4655, kaya 1108 na ina jumla ya vijiji vitano ambavyo ni Iyela-Nyara, Idunda, Tembela, Itewe na Isongwa.
Licha ya kata hiyo kuhudumia vijiji vitano lakini hadi sasa haina kituo cha afya na wananchi wake wanategemea kupata huduma katika zahanati moja tu ambayo ipo katika kijiji cha Idunda jambo ambalo linaathiri kuzorota kwa huduma ya afya katika kata hiyo.
Hata hivyo zahanati hiyo haina Miundombinu ambayo inakidhi mahitaji ya wagonjwa hasa akina mama wajawazito kwani ina vitanda viwili tu, ambapo kati yake kimoja kinatumika kwa ajili ya kujifungulia na kingine kwa ajili ya kupumzika.
Wanananchi hasa wanawake wanaoishi katika kata hiyo wanapaza sauti zao kwa kuiomba serikali kuwajengea kituo cha afya au kuboresha miundombinu ya zahanati hiyo ili waondokane na adha ya kutopata huduma bora za afya.
Wanawake hao walitumia mbinu ya igizo kufikisha kilio chao Mbele ya viongozi wa halmashauri ya Wilaya ya Mbeya ili waione changamoto yao, waichambue na kuifanyia utekelezaji kwa lengo la kuboresha huduma za afya katika kata yao hasa kwa mama na mtoto.
Kupitia igizo hilo walionesha namna akina mama wajawazito wanavyokuwa wanajifungulia njiani kutokana na kutembea umbali mrefu kufuata huduma ya afya hadi katika zahanati ya kijiji cha Idunda ambayo inahudumia kata nzima kutokana na kukosekana kwa kituo cha afya.
Pili Daniel, mkazi wa Itewe yeye aliigiza kama mama mjamzito akionesha uhalisia wa mazingira yao ambapo alionesha namna wanawake wajawazito wanavyojifungua njiani na wakati mwingine wanavyotozwa faini ya 10,000 na wahudumu wa afya kwa kosa la kujifungua njiani ama nyumbani.
Kupitia igizo hilo anasema umbali mrefu umekuwa ukisabaisha wanawake wa kata hiyo kujifungulia nyumbani au njiani au wakifika kwenye zahanati wanakosa sehemu ya kupumzikia kutokana na kukosekana kwa kitanda.
“Huko zahanati hata maji hakuna, tunatumia ya mtoni, wakati mwingine nesi anaenda kuchota au sisi wenyewe tunaenda mtoni kuchota ili yatusaidie wakati wa kujifungua,” alisema
Igizo hilo limebeba uhalisia wa maisha wanayopitia wananchi wa kata hiyo hasa wanawake, ambapo mkazi wa kata hiyo Wilbroa Ndezi ameongezea kwa kusema kuwa wakati mwingine wamekuwa wakikosa dawa wanapokuwa wamefika kwenye zahanati hiyo kwa ajili ya kupata matibabu jambo ambalo linapelekea waende kununua kwenye maduka ya watu binafsi kwa gharama kubwa.
Amesema licha ya kukata bima ya afya kupitia mfuko wa bima ya afya ya Taifa (CHF) kwa gharama ya sh.12,000 kwa mwaka au sh.6000 kwa  mtu mmoja bado wamekuwa wakikosa baadhi ya dawa.
“Kuna wakati unaona ni heri usiende zahanati, kule unaweza kufika ukaelezwa kuwa dawa hamna nenda kanunue kwenye duka la madawa la watu binafsi wakati wale wanaokuja kuandikisha bima walitueleza kila kitu tutakipata pale zahanati,” alisema.
Edda Mwalima amesema kuna wakati mama mjamzito akifika katika zahanati hiyo au Mgonjwa wa kawaida anakaa muda mrefu kusubiri huduma kutokana na uhaba wa watumishi na wakati mwingine anarudu nyumbani bila kupata huduma.
Amesema kukosekana kwa vitanda vya kupumzika kumekuwa kukisababisha baadhi ya wanawake wajawazito kutoona umuhimu wa kwenda zahanati na kuamua kujifungulia nyumbani jambo ambalo si salama kwa afya zao na watoto wao.
Kaimu Ofisa Mtendaji wa kata hiyo Michael mwaifweya anakiri kuwepo kwa changamoto hiyo na kueleza kuwa wameanza kujenga miundombinu Majengo kwa ajili ya kuongeza ukubwa wa utoaji huduma katika zahanati hiyo.
Amesema majengo hayo yanajengwa kwa nguvu za wananchi na kwamba yakikamilika yataondoa kero zilizopo na kuwa sasa wanatafuta eneo ambalo litajengwa kituo cha afya cha kata.
Mganga mkuu wa Zahanati hiyo, Angel Mabula amesema zahanati hiyo inawahudumu watatu na kwamba wanakidhi mahitaji ya wagonjwa kwa kuwa idadi ya wagonjwa wanaofika kupata huduma ya afya kwa siku ni wachache.
Amesema kwa siku wanawahudumia wagonjwa kwa wastani wa watu 5 hadi 3 na wakati mwingine 10 hadi 15  kulingana na majira ya hali ya hewa ambapo kwa wastani wa mwezi mmoja wajawazito 10 wanafika kliniki kwa ajili ya kufuatilia maendeleo ya mtoto.
“Kwa siku anaweza kuja mjamzito mmoja  hadi sita, lakini kwa watani wajawazito 100 wanafika kwa mwaka kuhudhuria kliniki, hapa kwenye zahanati kwa kweli hakuna msongamano wa wagonjwa licha ya kuwa kata ina zahanati moja, kwa sababu tumeweza kutoa elimu ya namna ya kuepukana na magonjwa yanayoweza kuzuilika na wagonjwa wengine wanaenda kituo cha afya Inyala,” amesema
Amesema kwenye chumba cha kujifungulia (Labour room) kuna vitanda viwili ambapo kimoja kinatumika kwa ajili ya kujifungulia na kingine kwa ajili ya kupumzika hivyo inapotokea wamepokea wagonjwa wengi inakuwa ni vigumu kuwamudu hivyo wengine wanalazimika kupumzika kwenye kitanda cha wagonjwa wa kawaida ambacho kipo kimoja.
Amesema kwa kuwa vijiji vingi vipo mbali na zahanati wakati mwingine wanalazimika kufanya kazi nje ya kituo kwa kuwafuata wananchi na kutoa huduma za kuwapima watoto na wanawake wajawazito na kwamba wameagiza kila kijiji kinunue kitanda na godoro kwa ajili ya kupumzikia wagonjwa.
Amebainisha kuwa kwa takwimu za mwaka 2017 wajawazito 48 walijifungulia kituoni hapo wakati tisa wakijifungulia njiani ama nyumbani ambapo kwa mwaka huo kiliripotiwa kifo cha mwanamke mmoja ambaye alijifungulia nyumbani.
“ Mwaka jana watoto sita chini ya umri wa mwezi mmoja walifariki dunia katika jamii hii,chini ya mwaka mmoja kifo kilikuwa kimoja na chini ya miaka mitano vifo vilikuwa n inane,” alisema
Amesema dawa zote muhimu zipo za kutosha katika zahanati hiyo na wakati mwingine zinapita muda wake wa matumizi (expire date) kutokana na idadi ndogo ya wagonjwa wanaofika katka zahanati hiyo.
Kaimu mkurugenzi wa halmashauri ya wilaya hiyo Zena Kapama amesema serikali inatatua changamoto za wananchi kutokana na kipaumbele chao walichokiibua kupitia mikutano yao na kamati ya maendeleo ya kata (WDC) na kuwasilishwa kwenye halmashauri.
Amesema kwa sasa wananchi wanapaswa kuibua mradi kulingana na huduma wanayohitaji na kuanza kuitekeleza na serikal jukumu lake ni kumalizia na kuleta watumishi kwa ajili ya kutoa huduma na kwamba suala la afya si kipaumbele kwa sasa kwani halijaletwa katika bajeti ya mwaka wa fedha 2018/19.
Hata hivyo serikali mkoani Mbeya imeanza mikakati maalumu ya kuimarisha afya ya msingi kwa wananchi ili kuimarisha nguvu kazi kwa ajili ya shughuli za kijamii na kiuchumi  ikiwemo ujenzi wa Viwanda na shughuli za kilimo.
Moja ya mikakati iliyoanzishwa na Serikali hiyo ni Mkuu wa Mkoa huo, Amos Makalla, kuwafunga vitanzi wakuu wa Wilaya zote za Mkoa huo kwa kuwasainisha Mkataba maalumu wa uhamasishaji wa ujenzi wa vituo vya Afya kwenye kila Kata, ujenzi wa Zahanati kila kijiji na kuwahamasisha wananchi kujiunga na Mfuko wa Afya ya Jamii (CHF).
Mkataba kama huo ulisainiwa kati ya Kaimu Katibu Tawala wa Mkoa wa Mbeya, Nyasebwa Chimagu na wakurugenzi watendaji wa Halmashauri zote za Mkoa huo.
Akizungumza na wakuu wa Wilaya, wakurugenzi wa Halmashauri zote, Waganga wakuu wa Wilaya na maofisa watendaji wa Kata zote za Mkoa wa Mbeya , Makalla amesema mkataba huo unawasisitiza viongozi hao kwenda kuwahamasisha wananchi kujenga maboma ya vituo vya Afya kwenye Kata zao na Zahanati kwenye vijiji ili Serikali imalizie kwenye uezekaji.
Amesema Mkoa wa Mbeya una jumla ya Kata 178 lakini zenye vituo vya Afya ni 25 pekee, huku vijiji 300 kati ya 533 ndio vikiwa havina zahanati kama inavyotakiwa.
“Hatuwezi tukawa tunasema Hapa kazi tu! Na kusisitiza uchumi wa viwanda wakati wananchi wetu hawana uhakika wa kupata huduma za afya jirani na maeneo yao, hivyo Mkataba huu utamlazimisha kila mtu kuhakikisha tunaimarisha afya za watu wetu,” amesema Makalla.
Hata hivyo amesema ili kuweka msisitizo wa Mkataba huo nakala zake atazituma kwa Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Ummy Mwalimu, Waziri wa Ofisi ya Rais Tawala za mikoa na Serikali za mitaa, Sulemani Jafo na Makatibu wakuu wa Wizara hizo.
Makala amesema watahakikisha wanahamasisha wananchi kwa kuanzia na viongozi wao ili mpaka kufikia mwaka 2020 kila kijiji kiwe tayari kina Zahanati, kila Kata iwe na Kituo cha Afya na asilimia 100 ya wananchi wawe wamejiunga na Mfuko wa Afya ya Jamii (CHF).
Mwisho.

No comments:

Post a Comment